Rea yatenga bilioni 10 kusambaza mitungi ya gesi vijijini

Wakala wa Nishati Vijijini (REA), katika Mwaka huu wa Fedha (2023/24), umetenga shilingi bilioni 10 kwa ajili ya kusambaza mitungi ya gesi ya LPG, majiko na vifaa vyake katika maeneo ya vijijini kwa njia ya ruzuku.

Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Hassan Saidy ameyasema hayo wakati akiwasilisha Taarifa ya Wakala kwa Naibu Waziri wa Nishati, Judith Kapinga, Novemba 7, 2023.

Alisema kuwa, kiasi cha mitungi kati ya 200,000 hadi 500,000 inatarajiwa kusambazwa katika maeneo ya vijijini kutegemea kiwango cha ruzuku kitakachotolewa.

Akielezea Mradi wa usambazaji gesi ya kupikia kwa ujumla, Mhandisi Saidy alisema unategemewa kusambaza mitungi ya gesi 70,020 ambapo hadi kufikia Agosti 15 mwaka huu, mitungi 23,806 (sawa na asilimia 34) ilikuwa imeshasambazwa kwa wananchi mbalimbali kupitia kwa Wabunge ambao ni wawakilishi wao.

“Lengo la Serikali kupitia REA katika utekelezaji wa Mradi huo ni kuhamasisha matumizi ya nishati safi na salama ya kupikia katika maeneo yao,” alifafanua.

Aidha, Mkurugenzi Mkuu alieleza kuwa, katika hatua nyingine, REA inatekeleza Mradi wa usambazaji gesi asilia kwa ajili ya kupikia katika mikoa ya Lindi na Pwani kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), ambapo alisema Mkataba umesainiwa na maombi ya fedha za awali, yapo Wizara ya Fedha kwa ajili ya uhakiki.

Share: