
Mbunge wa Jimbo la Dodoma Mjini Mh. Anthony Mavunde amezindua Ushirika wa waendesha Pikipiki na Bajaj Dodoma na kuwataka wasafirishaji hao kutumia fursa hiyo kujiimarisha kiuchumi kupitia mikopo mbalimbali.
“Ninawapongeza kwa uamuzi huu wa kuanzisha SACCOS yenu,ni wakati muafaka sasa kuwaona vijana mkimiliki vyombo vya usafiri vya kwenu wenyewe.
Kupitia SACCOS hii vijana wengi watabadilisha maisha yao na kujijenga kiuchumi.
Nitoe rai kwa viongozi wa SACCOS kuhakikisha mnatumia vizuri mkopo wa asilimia 10 wa mapato ya ndani ya Jiji la Dodoma ambapo mpaka sasa zimetengwa shilioni Bilioni 7 kwa ajili ya kukopesha vikundi vya wakina mama,vijana na watu wenye ulemavu”Alisema Mavunde.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Alhaj Jabir Shekimweri anewataka maafisa wasafirishaji hao kutumia SACCOS kutatua changamoto za msingi za kiuchumi za vijana wengi na kuahidi kwamba serikali itakuwa nao bega kwa bega kuhakikisha inaweka mazingira rafiki ya ufanyaji wa shughuli zao.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Dodoma SACP George Katabazi amewataka maafisa wasafirishaji hao kuzingatia sheria za usalama barabarani na kwamba Jeshi la Polisi litaendelea kushirikiana nao kwa karibu kama wadau muhimu wa usalama katika jamii.
Akitoa shukrani zake Mwenyekiti wa UMAPIDO Ndg. Marwa Chacha Nyagate ameshukuru Mh. Rais Dkt. Sania S. Hassan kwa kuwajengea ofisi za chama hicho mkoani Dodoma na pia kumshukuru Mbunge Mavunde kwa mchango wa Tsh 15,000,000 kuiwezesha SACCOS yao kuanzishwa na kuahidi kwamba wataitumia SACCOS kuleta mageuzi ya kiuchumi kwa vijana wote waliopo kwenye tasnia hiyo.Mwenyekiti Marwa pia alisisitiza umuhimu wa vijana hao kushiriki uchaguzi mkuu 2025 ili kutimiza takwa la kikatiba.