Mashamba ya miwa yameharibika na mvua tutaagiza sukari nje

Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe amesema kwa mwaka huu Serikali itaingiza nchini zaidi ya tani laki tatu za sukari ili kukabilana na upungufu wa sukari nchini.

Amesema hadi kufikia Machi 15, 2024, tani 60,000 za sukari zitakuwa zimeingizwa nchini na hivyo kuleta unafuu kwa watumiaji.

Waziri Bashe amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuagiza sukari kutoka nje kutokana na mashamba mengi ya miwa kuathiriwa na mvua na hivyo kuathiri uzalishaji.

Amesema Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) ndio imeingia makubaliano na kampuni zinazoingiza sukari nchini na si wafanyabishara.

Hata hivyo, Waziri Bashe amesema tatizo lililopo sasa ni baadhi ya wafanyabiashara kuongeza bei ya sukari na mpaka sasa zaidi ya wafanyabiashara 80 wamekamatwa kwa kuongeza bei ya sukari.

Waziri Bashe ameyasema hayo Ikulu, Dar es Salaam wakati wa mkutano wa wahariri wa wabari na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu kuhusu ziara ya Rais Samia Suluhu Hassan huko Vatican, Norway pamoja na Addis Ababa, Ethiopia.

Share: