Bashungwa atoa siku 7 kwa crg7 kuja na mpango kazi wa kukamalisha miradi.

Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa ametoa siku saba kwa Mkandarasi Kutoka China, China Railway Seventh Group Ltd (CRG7) kuwasilisha Wizarani mpango kazi wa miradi mitano anayoitekeleza hapa nchini kutokana na utekelezaji wa miradi yote kusua sua na kuwa nyuma ya muda wa mikataba.

Ametoa maelekezo hayo wakati alipokutana na Uongozi wa juu wa Kampuni hiyo, ulioongozwa na Mkurugenzi mkuu Msaidizi wa Kamapuni ya CRG7 Kutoka China, ndugu Xianyang Dong.

Bashungwa amemtaka Mkurugenzi mkuu huyo wa CRG7 kuhakikisha anawasilisha kwake Mpango kazi wa kila Mradi na namna alivyojipanga kukamilisha, kutokana na kutoridhishwa na kasi ya utekelezaji wa miradi yote mitano waliyopewa kujenga hapa nchini.

Ameeleza kuwa Mkandarasi CRG7 anatekeleza miradi mitano ambayo ni Ujenzi wa Kiwango cha lami barabara ya Amanimakoro - Ruanda km 35 iliyopo mkoani Ruvuma ambapo utekelezaji wake ulitakiwa kuwa asilimia 92 lakini sasa umefikia asilimia 24.

Aidha, Ameeleza Ujenzi wa Kiwango cha lami barabara ya Kibaoni - Mlele junction km 50 iliyopo mkoani Katavi ambapo walitakiwa kuwa asilimia 26 lakini sasa wamefikia asilimia 12.

Amebainisha miradi mingine ambayo utekeleaji wake haujaanza ni barabara ya Nyamwage - Utete km 33.7 mkoani Pwani, Ujenzi wa Daraja la mpiji chini na barabara unganishi ya km 2.3 vilivyopo mkoa Dar es Salaam.

Kadhalika, Bashungwa amemuagiza Mtendaji Mkuu wa TANROADS kuondokana na hali ya kutoa miradi mingi ya ujenzi kwa Mkandarasi mmoja, jambo linalosababisha miradi kushindwa kutekelezwa kwa wakati kulingana na mikataba.

Share: