Mara: mhasibu wa halmashauri ya serengeti ahamisha milioni 150 kwa basi

Leo imeingia siku ya tatu kati ya siku 5 za ziara ya Waziri Mkuu Majaliwa katika Mkoa wa Mara ambapo moja ya makubwa aliyoyaibua kwenye ziara hiyo ni pamoja na hii ya tuhuma za Mkuu wa kitengo cha Fedha na Uhasibu wa Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti Saad Mutunzi Ishabailu kudaiwa kuhamisha milioni 213 na kuzitumia kwa matumizi yao binafsi yeye na Watumishi wengine wa Ofisi ya Rais TAMISEMI.

“Ilipofika June 30 walikuwa wamemaliza kutumia fedha hizo na ikabakia milioni 9 lakini kwa kuwa walishaandika barua ya kuomba kibali, bado fedha hizo zilihamishwa na kuingizwa kwenye akaunti ya Halmashauri June 19, 2023 na aliyejua alikuwa Ishabailu pekee, hakutoa tarifa kwa Mkurugenzi, Mwenyekiti wala Wakuu wa Idara” Majaliwa.

“Nilituma timu yangu hapa ije kufanya uchunguzi, ikawahoji baadhi ya Watumishi akiwemo Afisa Mipango wa Halmashauri, Wilfred Mwita ambaye alisema hajui uwepo wa hizo fedha wala hawakuwa na mpango wala bajeti inayohitaji hizo fedha, Mkurugenzi wa sasa Furaha alipoulizwa naye alisema hajui uwepo wa hizo fedha kwani alianza kazi Agosti mwaka jana.”

Waziri Mkuu Majaliwa amesema June 21, mwaka jana Ishabailu alianza kufanya matumizi ya hizo fedha kwa kushirikiana na Mfanyabiashara wa Mugumu Daudi Matinde Chacha kupitia kwenye akaunti zake za Benki mbili tofauti kwa kupitia miamala minne ya sh. milioni 76.3, sh. milioni 57.7, Tsh. milioni 47 na Tsh.milioni 32.5 na alipoulizwa na timu ya uchunguzi Matinde alikiri kuwa haidai fedha yoyote Halmashauri ya Serengeti isipokuwa Mweka Hazina huyo aliomba apitishie fedha zake kwenye akaunti zake kwa sababu zinahitajika haraka kwa matumizi ya Ofisi.

“Aliambiwa atoe shilingi milioni 189 akamkabidhi zote Ishabailu na zilizobakia (sh. milioni 24) akaambiwa abaki nazo ambapo baada ya kupokea fedha hizo Ishabailu alipanda basi kutoka Serengeti hadi kituo cha Mabasi cha Nyegezi, Mwanza na kumkabidhi Zablon Mponzi ambaye alisema zinatakiwa haraka na wakubwa huko Dodoma bila kuwataja wakubwa hao ni akina nani, yeye pia alikabidhi shilingi 150 kwa huyo Zablon ina maana alibakia na sh. milioni 39.” Majaliwa.

Share: