Nchi kadhaa zimewataka raia wao kuondoka lebanon huku hofu ikiongezeka ya mzozo mkubwa katika mashariki ya kati.

Iran imeapa kulipiza kisasi "kikali" dhidi ya Israel, baada ya kifo cha mkuu wa kisiasa wa Hamas Ismail Haniyeh huko Tehran siku ya Jumatano, Israel haijasema chochote.

Mauaji yake yalikuja saa chache baada ya Israel kumuua kamanda mkuu wa Hezbollah Fuad Shukr huko Beirut.

Maafisa wa nchi za Magharibi wanahofia kwamba Hezbollah, wanamgambo wanaoungwa mkono na Iran na vuguvugu la kisiasa lenye makao yake makuu nchini Lebanon, linaweza kuwa na jukumu muhimu katika ulipizaji kisasi wa aina hiyo, ambao nao unaweza kuibua shambulio kali la Israel.

Juhudi za kidiplomasia za Marekani na nchi nyingine za Magharibi zinaendelea kujaribu kupunguza mvutano katika eneo hilo.

Idadi inayoongezeka ya safari za ndege zimekatishwa au kusimamishwa katika uwanja wa ndege pekee wa kibiashara huko Beirut.

Marekani, Uingereza, Australia, Ufaransa, Canada, Korea Kusini, Saudi Arabia, Japan, Uturuki na Jordan ni miongoni mwa nchi zilizowataka raia wao kuondoka Lebanon haraka iwezekanavyo.

Hofu ya kuongezeka kwa uhasama ambao unaweza kuikumba Lebanon ni kubwa zaidi tangu Hezbollah ilipoanza mashambulizi yake dhidi ya Israel, siku moja baada ya mashambulizi mabaya ya Hamas kusini mwa Israel tarehe 7 Oktoba, kuwaunga mkono Wapalestina huko Gaza.

Share: