Mtoto wa rais wa somalia anatakiwa uturuki kwa mashtaka yaliyopelekea kifo

Waziri wa sheria wa Uturuki ametangaza Alhamisi kwamba mtoto wa kiume wa Rais wa Somalia Hassan Sheikh Mohamud, anatarajiwa kurejea Uturuki kujibu mashtaka ya ajali mbaya ya barabarani iliyosababisha kifo mjini Istanbul.

Yilmaz Tunc, waziri wa sheria wa Uturuki, aliwaambia waandishi wa habari kwamba Ankara ilifanya mazungumzo na mamlaka ya mahakama ya Somalia juu ya kumrudisha Mohamed Hassan Sheikh Mohamud. “Katika siku zijazo, mshtakiwa atakuja Uturuki, na mchakato wa kesi utafanyika”, Tunc alisema.

Hapo Novemba 30, Mohamud alimgonga Yunus Emre Gocer, mwendesha pikipiki katika wilaya ya Fatih huko Istanbul, wakati mtoto huyo wa Rais akiendesha gari yenye namba za leseni ya kidiplomasia. Muathirika huyo mwenye umri wa miaka 38 alipelekwa hospitali mara moja, ambako alifariki Disemba 6.

Kulingana na nyaraka za polisi ambazo VOA, Idhaa ya Kituruki ilizipata, baada ya kutoa ushahidi, Mohamud aliachiliwa siku hiyo hiyo ya ajali kwa maelekezo ya mwendesha mashtaka wa Istanbul.

Share: