Dar es salaam: january hadi february 2024 makosa yaliyokutwa kwenye pikipiki ni 36,775

Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam limekamata pikipiki zilizoibwa

maeneo mbalimbali ya Dar es salaam na Mikoa ya jirani ambapo kupitia operesheni hiyo iliyoanza February 06, 2024 wamemkamata Omari Mlopa (28) Mkazi wa Mlandizi na wenzake wawili wakiwa na pikipiki 32 zilizoibwa na baadae kuzifanya zao kwa kuzikodisha kwa mikataba kwa Watu mbalimbali na kujipatia pesa kila siku.

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam, Muliro Jumanne amesema “Uchunguzi wa awali uliofanywa na Jeshi la Polisi umebaini kuwa Watuhuhumiwa hao walibadilisha namba za usajili za pikipiki hizo na kuweka namba bandia ili zisitambulike na pikipiki 13 tayari zimetambuliwa na Wamiliki”

“Wakati huohuo Jeshi la Polisi Kanda maalum ya Dar es salaam linaendelea operesheni maalum ya ukamataji wa Watu wanaokiuka sheria kwa kutenda makosa ya usalama barabarani hasa kwa waendesha pikipiki (Bodaboda) na Bajaji ambapo katika kipindi cha January hadi December 2023 makosa ya pikipiki yaliyokamatwa ni 179,174, walioandikiwa faini za papo kwa hapo ni 178,937, waliofikishwa Mahakamani ni 237, waliohukumiwa adhabu ya kulipa faini 236, na mmoja alihukumiwa kifungo jela

“Kwa kipindi cha January hadi February 2024 makosa yaliyokutwa kwenye pikipiki ni 36,775, walioandikiwa faini za papo kwa hapo ni 36,754, waliofikishwa Mahakamani ni 14 na mashauri 7 yapo kwenye ofisi ya Mashitaka ya Taifa”

Share: