Tume ya mipango shirikisheni wananchi uandaaji dira ya maendeleo ya taifa 2050 - dkt.biteko

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko ameagiza Tume ya Mipango nchini kuweka uratibu wa ushiriki wa makundi mbalimbali ya wananchi na Wadau wengine katika kutoa maoni kwenye mchakato unaoendelea wa uandaaji Dira ya Maendeleo ya Taifa ya mwaka 2050.

Amesema hayo wakati akimwakilisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Kassim Majaliwa Majaliwa,katika hafla ya ufunguzi wa Kongamano la kwanza Wanamipango 2023 iliyofanyika tarehe 27 Novemba 2023 jijini Arusha.

"Tume ya Mipango hakikisheni Wananchi wote wanashiriki kikamilifu kutoa maoni yao kuhusu Tanzania wanayoitaka katika miaka 25 ijayo, maandalizi ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050 yameanza na kutokana na umuhimu wa Dira kwa Taifa letu, wanamipango na wadau wote ni muhimu kila mmoja kwa nafasi yake ashiriki kikamilifu katika hatua zote za maandalizi kama atakavyohitajika." Amesisitiza Dkt. Biteko

Suala jingine alilosisitiza ni kwa Maafisa Mipango kubadilika na kufanya ufuatiliaji na tathmini ya Miradi na Programu zote zinazotekelezwa katika maeneo yao ikiwemo zinazofadhiliwa na Wadau wa Maendeleo badala ya ile inayogharamiwa na Serikali Kuu au Halmashauri pekee.

Vilevile, Dkt. Biteko ameelekeza Wakurugenzi wa Mipango kuzingatia utamaduni wa kuwa na mawazo ya pamoja katika kupanga mipango ya Serikali na nchi kwa ujumla ili kuleta mipango imara itakayosaidia Taifa kufikia uchumi wa juu.

Suala jingine alilosisitiza Dkt. Biteko ni Wanamipango waliopewa jukumu la kusimamia miradi pamoja na ufuatiliaji na tathmini kuzingatia utaratibu wa kutoa taarifa za utekelezaji wa programu na miradi ya maendeleo inayotekelezwa.

Share: