Rais william ruto thuluthi mbili ya jinsia imetekelezwa kikamilifu katika chama chake (uda)

Rais William Ruto Alhamisi amesisitiza kwamba ataendelea kujitolea kuhakikisha kuwa sheria ya thuluthi mbili ya jinsia imetekelezwa kikamilifu katika chama chake cha United Democratic Alliance (UDA) na katika serikali ya Kenya Kwanza kwa jumla.

Wakati wa uzinduzi wa Mkakati wa Baraza la Magavana Wanawake G7 jijini Nairobi, Ruto alisema kuwa serikali yake imefuata mikakati mikali ili kutimiza kiwango cha ujumuishaji wa kijinsia katika katiba na atakuwa mstari wa mbele kuonyesha kwa mfano alichosema.

“Wakati Riggy G (Naibu rais Rigathi Gachagua) na mimi tukikubaliana jinsi mambo yatakavyokuwa siku za usoni lazima pia tukubaliane kwamba kwenda mbele ikiwa mwanamume ni mgombea wa urais mwanamke lazima awe mgombea mwenza na ikiwa mwanamke ni mgombea, mwanamume anafaa kuwa mgombea mwenza," Ruto alisema katikati ya umati wa watu waliokuwa wakishangilia.

Aliongeza: "Lazima tufanye kwa kukusudia kuhusu hilo vinginevyo halitatokea kamwe."

Ruto alisema kuwa hayo pia yanafaa kufanywa kuwa ya lazima kwa Magavana na nyadhifa zote za uongozi ndani ya chama.

Alionyesha imani kuwa viongozi wengine wa chama watapokea vyema pendekezo la kufanikisha kikamilifu kanuni ya thuluthi mbili ya jinsia.

Share: