Mtatiro akabidhiwa mikoba shinyanga

Aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, Wakili Julius Mtatiro ameripoti kwenye kituo chake kipya cha kazi ili kuanza majukumu ya Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga.

Katika kikao kifupi cha makabidhiano ya ofisi, kilichohudhuriwa na Kamati ya Usalama ya Wilaya hiyo na Wakurugenzi 2; Manispaa na Shinyanga Vijijini, DC Mtatiro amekabidhiwa nyaraka mbalimbali, zikiwemo Taarifa ya Wilaya, Katiba ya Tanzania, Ilani ya CCM 2020 - 2025.

Mkuu wa Wilaya ya Misungwi mkoani Mwanza Bi. Johari Samizi ambaye amehudumu kama DC Shinyanga kwa kipindi cha mwaka mmoja, ndiye amemkabidhi ofisi na mamlaka kwa DC Mtatiro.

DC Mtatiro amesema ameridhishwa na kasi ya maendeleo inayoendelea wilayani Shinyanga na kwamba anajipanga kushirikiana kwa dhati na viongozi, wadau na wananchi wote ili kazi ya Mkuu wa Mkoa na Rais Samia iwe nyepesi.


Mtatiro ameahidi kuja na mpango kazi kabambe ambao utaendelea kuipaisha Wilaya ya Shinyanga na wananchi wake kiuchumi huku akisisitiza kuwa kipaumbele chake ni "haki" za wananchi.

Mara baada ya makabidhiano hayo, DC Mtatiro ameanza safari kuelekea Tunduru mkoani Ruvuma ili kukabidhi Ofisi ya DC Tunduru kwa Mkuu wa Wilaya hiyo wa sasa, Simon Chacha, ambaye kabla alikuwa DC Sikonge, mkoani Tabora.

Share: