Mhe. simbachawene awakumbuka walimu na manesi, aitaka taasisi ya watumishi housing investment kuwajengea makazi bora

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene ameitaka Taasisi ya Watumishi Housing Investments (WHI) kuja na ubunifu wa kujenga makazi bora ya watumishi wa umma katika maeneo ya mijini jirani na maeneo ya shule na hospitali ili kuwaondolea changamoto ya makazi manesi na walimu kwa lengo la kuboresha utendaji kazi wao 

Amesema maeneo ya mijini, shule pamoja na hospitali zinamiliki maeneo makubwa ambayo Taasisi ya WHI inaweza kuyatumia kujenga majengo marefu kwenda juu ili kuwafanya walimu na manesi wafurahie kutoa huduma kwa wananchi kwa kuishi kwenye makazi bora jirani na maeneo ya kazi 

Mhe. Simbachawene ametoa kauli hiyo leo Jijini Dar es Salaam alipokuwa akizungumza na Timu ya Menejimenti ya Taasisi ya Watumishi Housing Investments (WHI) ikiwa ni muendelezo wa kusikiliza changamoto zinazoikabili Taasisi anazozisimamia pamoja na kufuatilia utekelezaji wa maagizo aliyoyatoa wakati wa ziara aliyoifanya Mwezi Agosti mwaka jana

Amesema katika maeneo ya mijini watumishi wakiwemo walimu na manesi wamekuwa wakilazimika kutafuta makazi mbali na maeneo wanakofanyia kazi kwa vile ni vigumu kupata nyumba karibu na maeneo hayo na hata makazi yakipatikana gharama zake za kulipia huwa ni kubwa kulingana na kipato chao.

'' Hakuna asiyejua umuhimu wa walimu na manesi katika nchi hii lakini lakini wengi wa wamekuwa wakiishi maeneo ya mbali na wanakofanyia kazi na hivyo kulazimika kulipa nauli kubwa kwa vile hawawezi kumudu kulipa kodi ya makazi yaliyo jirani na maeneo yao ya kazi, waguseni hawa kwa kuwajengea makazi bora. amesema Mhe. Simbachawene

Mhe.Simbachawene amesisitiza kuwa Nyumba zikiwa jirani na eneo la kazi inasaidia kupunguza gharama za maisha na kuongeza ufanisi kazini na hilo ndio lengo haswa la Serikali ya awamu ya sita kuhakikisha watumishi wanafurahia mazingira ya kazi kwa gharama rafiki"

Amesema Watumishi wa Umma wakiwemo walimu na manesi wanaofanya kazi katika maeneo ya mijini wamekuwa wakilazimika kusafiri umbali mrefu kutokana na changamoto ya makazi na hivyo kupelekea kutoa huduma zisizoridhisha kwa wateja wao.

Mhe. Simbachawene amesema kitendo cha watumishi wa umma kutokuwa na makazi bora na kuwa mbali na maeneo yao wanayofanyia kazi ni changamoto kubwa inayoathiri utendaji kazi, hivyo ameitaka taasisi hiyo kuona umuhimu wa kufanya hivyo kwani utekelezaji wq ilani ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2020/ 2025  

Mhe. Simbachawene amesema ujenzi wa makazi bora hayo karibu na maeneo ya kazi, kutawasaidia watumishi wanaoajiriwa kwa mara ya kwanza maeneo kutohangaika. “Mkijenga nyumba maeneo ya jirani na vituo vya kazi, kutawasaidia sana watumishi kutoichukia kazi kwa watapata sehemu nzuri ya kuishi,” Mhe. Simbachawene amesisitiza.

Share: