Mashambulizi ya Marekani dhidi ya makundi yenye uhusiano na Iran nchini Syria na vita vya Gaza

Waziri wa Ulinzi wa Marekani Lloyd Austin amesema kuwa Marekani ilianzisha mashambulizi siku ya Jumapili "katika vituo vya mashariki mwa Syria vinavyotumiwa na kikosi cha Iran Revolutionary Guard na makundi yenye uhusiano na Iran."

Aliongeza katika taarifa yake, "Mashambulizi yaliyofanywa dhidi ya kituo cha mafunzo na nyumba salama karibu na miji ya Al-Bukamal na Al-Mayadin, mtawalia, yanafanyika kujibu mashambulizi yanayoendelea dhidi ya majeshi ya Marekani nchini Syria na Iraq".

Mashambulizi hayo ya Marekani yalisababisha mauaji ya wapiganaji wanane wanaoiunga mkono Iran, kulingana na kile kilichoripotiwa na Shirika la Kuchunguza Haki za Kibinadamu la Syria, lenye makao yake makuu katika mji mkuu wa Uingereza, London.

Shirika hilo lilisema, "Idadi ya waliofariki ni 8, ikiwa ni pamoja na takriban raia mmoja wa Syria, pamoja na Iraq."

Kulingana na shirika la uangalizi la Syrian Observatory "mashambulizi ya anga yalilenga ghala la silaha katika mji wa Hasrat katika mashamba ya Albukamal. Shambulio hilo lilisababisha uharibifu kamili wa ghala hilo, na milipuko ya mfululizo ilisikika kutokana na kuchomwa kwa risasi katika ghala."

Ndege hiyo pia ilifanya uvamizi mmoja, ambapo ililenga sehemu ya kurushia makombora katika mashamba ya Haidariya karibu na mji wa Al-Mayadeen."

Taarifa ya Waziri wa Ulinzi ilisema kwamba mashambulizi hayo yalifanyika ndani ya mfumo wa "kujilinda," na kuongeza, "Rais Biden hana kipaumbele cha juu zaidi ya usalama wa wafanyakazi wa Marekani. Ameamuru kuchukuliwa hatua leo ili kuweka wazi kwamba Marekani itajilinda yenyewe, watu wake na maslahi yake.

Hii ni mara ya tatu, katika muda wa chini ya wiki tatu, ambapo jeshi la Marekani limelenga maeneo nchini Syria ambayo inasema yana uhusiano na Iran.

Siku ya Jumatano, Marekani ilianzisha mashambulizi katika kile ilichosema ni maeneo mawili ya kuhifadhi silaha yanayotumiwa na walinzi wa kikosi cha Iran Revolutionary Guard na vikosi vyake tanzu katika eneo la Maysalun mashariki mwa Syria.

Mnamo Oktoba 26, pia ililenga vituo viwili ambavyo ilisema vinatumiwa na Iran na washirika wake nchini Syria.

Washington ilisema kuwa idadi ya mashambulizi yaliyofanywa na makundi yenye silaha yenye mafungamano na Iran dhidi ya majeshi ya Marekani nchini Syria na Iraq ilifikia zaidi ya mashambulizi 45 tangu Oktoba 17, na kusababisha kujeruhiwa kwa makumi ya wanajeshi wa Marekani.

Kuna makumi ya makundi yanayofanya mashambulizi ya kijeshi dhidi ya vikosi vya muungano wa kimataifa, unaoongozwa na Marekani ndani ya mfumo wa muungano kati ya serikali ya Syria na Iran, mashuhuri zaidi kati yao ni: Kikosi cha Quds, Hezbollah kutoka Lebanon, Hezbollah cha Iraq, kikondi cha Nujaba na Asaib Ahl al-Haq.

Kwa kuongezea, kuna vikundi vingine vya Iraq kama vile Brigedia ya Abu al-Fadl al-Abbas, Brigedia ya Badr, na vikundi vingine vinavyofadhiliwa na wanajeshi wa Iraq pamoja na kikundi cha Fatimiyyin cha Afghanistan na kikundi cha Zainabiyyin cha Pakistani ambacho kilifanya kazi moja kwa moja chini ya uongozi wa Kikosi cha Quds katika vita vingi ambavyo jeshi la Syria lilipigana huko Aleppo na maeneo ya Deir ez-Zor

Kuenea kwa vikundi hivi hakukomei mashariki mwa Syria ambapo mashambulizi ya Marekani yalitokea, lakini pia inaenea hadi maeneo mengine katika jiografia nzima ya Syria.

Lakini Deir ez-Zor na mji wa Al-Bukamal, ulio kwenye mpaka na Iraq, ndio mahali pa mkusanyiko wake, na wataalam na waangalizi wanauelezea kama "mji mkuu wa Revolutionary Guard.

Makadirio yanatofautiana kuhusiana na idadi ya wanachama wa makundi yanayounga mkono Iran waliotumwa nchini Syria, lakini baadhi ya wataalamu wanakadiria idadi yao kati ya wapiganaji elfu 25 na 40, na idadi hii inaweza kuongezeka au kupungua kulingana na mahitaji.

Kuongezeka kwa mashambulizi dhidi ya vikosi vya Marekani katika wiki za hivi karibuni kunahusishwa na vita kati ya Israel na Hamas, ambayo ilianza wakati vuguvugu hilo lilipofanya shambulio ambalo halijawahi kushuhudiwa katika mpaka kati ya Ukanda wa Gaza na Israel mnamo Oktoba 7, ambalo kwa mujibu wa maafisa wa Israel, liliua takriban watu 1,200.

Ingawa matukio haya si mapya na yametokea nyakati tofauti huko nyuma, kutokea kwao wakati kama huo kulionyesha "kitu kingine kisichokawaida."

Iliendana na Marekani kutuma vikosi vya kijeshi na meli mbili za kubeba ndege katika eneo la mashariki mwa Mediterania ili kuisaidia Israel katika vita inayoendesha dhidi ya Hamas katika Ukanda wa Gaza

Hii ilifuatiwa na mfululizo wa taarifa zilizotolewa na makundi yanayoungwa mkono na Iran, yakitishia kujibu kwa kulenga vituo vya Marekani.

Takriban wanajeshi 2,500 wa Marekani wako nchini Iraq na takriban wanajeshi 900 nchini Syria ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuzuia kurejea kwa kile kinachojulikana kama Dola la Kiislamu.

Vita vya Gaza vilikuwa na madhara kwa Marekani nje ya Iraq na Syria, huku Wahouthi walio karibu na Iran wakitangaza wiki iliyopita kwamba waliiangusha ndege isiyo na rubani ya Marekani kwenye pwani ya Yemen, ambayo walisema ilikuwa inafanya kazi ndani ya mfumo wa Marekani wa utoaji wa msaada wa kijeshi kwa Israeli.

Afisa mkuu katika Wizara ya Ulinzi ya Marekani alithibitisha kuwa ndege isiyo na rubani ya MQ-9 ya Marekani ilitunguliwa katika pwani ya Yemen

Share: