Makamu wa rais dkt. philip mpango ameongozana na viongozi mbalimbali wa mkoa wa dar es salaam katika zoezi la usafi wa mazingira soko la ilala

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango ameongoza viongozi pamoja na wananchi mbalimbali wa Mkoa wa Dar es Salaam katika zoezi la usafi wa mazingira lililofanyika Soko la Ilala linalotumika kwa biashara mbalimbali ikiwa ni kuelekea katika Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani.

Akizungumza mara baada ya kufanya usafi, Makamu wa Rais amewataka Watanzania kujenga utamaduni wa kufanya usafi wakati wote. Amesema katika hatua za utafutaji Maisha ni vema kukumbuka suala la usalama katika maeneo ya shughuli za kiuchumi ikiwemo kufanya usafi na kukusanya taka katika sehemu sahihi.

Makamu wa Rais ametoa wito kwa watanzania wote kufanya jitihada katika kupiga vita utupaji taka ovyo. Amewataka Viongozi katika ngazi zote kuhakikisha wanatoa elimu kwa wananchi na kuwajengea tabia ya kupenda kufanya usafi.


Amemtaka Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam kuhakikisha fedha zinazotarajiwa kutoka Benki ya Dunia zinatumika katika ujenzi wa madampo ya kisasa yatakayosaidia katika urejerezaji taka kama ilivyopangwa. Pia ametoa rai ya kuanzishwa kwa mashindano ya usafi katika Wilaya za Dar es salaam ili kuwa motisha ya ufanyaji usafi mkoani humo.

Pia ameagiza Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Dar es salaam (DAWASA) kuhakikisha inadhibiti maji machafu yanayotiririka katika Soko la Ilala ndani ya wiki moja.

Usafi huo pia umeshirikisha viongozi mbalimbali akiwemo Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Mussa Zungu, Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Khamis Hamza Khamis, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Albert Chalamila, Wakuu wa Wilaya, Viongozi wa Taasisi mbalimbali pamoja na Chama Cha Mapinduzi.

Share: