Korea kaskazini yarusha kombora lengine la masafa mafupi

Jeshi la Korea Kusini limesema leo kuwa Korea Kaskazini imerusha kombora la pili la masafa mafupi ndani ya bahari katika pwani yake ya mashariki.

Katika taarifa, jeshi la Korea Kusini limeeleza kuwa kombora hilo limerushwa mapema leo asubuhi bila ya kutoa maelezo zaidi ya umbali wake.

Wizara ya ulinzi ya Japan imesema pia imegundua kile wanachokishuku kuwa kombora la masafa mafupi lililorushwa na Korea Kaskazini.

Urushaji huo umetokea saa chache tu baada ya Korea Kusini kuripoti kwamba jirani yake Korea Kaskazini inafanya jaribio la kurusha makombora ya masafa mafupi ndani ya bahari, katika kile kinachoonekana ni kuanza tena majaribio ya silaha.

Wachambuzi wamesema hatua ya Korea Kaskazini ya kufanya majaribio ya silaha ni njia mojawapo ya kupinga hatua ya Korea Kusini na Marekani kuimarisha mipango yao ya silaha za nyuklia katikati ya vitisho vya nyuklia vya Pyongyang.

Share: