Korea kaskazini imetuma zaidi ya maputo 1,500 yaliyojaa takataka nchini korea kusini katika kile kinachoaminika kuwa kulipiza kisasi

Wizara ya Muungano ya Korea Kusini ilitangaza tarehe 24 kwamba vimelea vinavyotokana na kinyesi cha binadamu na nguo zilizoharibika za Hello Kitty zilipatikana kwenye takataka zilizokutwa kwenye mfuko kwenye puto lililotumwa na Korea Kaskazini kwenda Korea Kusini.

Tangu Mei, Korea Kaskazini imetuma zaidi ya maputo 1,500 yaliyojaa takataka nchini Korea Kusini katika kile kinachoaminika kuwa kulipiza kisasi kwa wakosoaji wa kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong Un kutuma vipeperushi nchini humo.


Mamlaka ya Korea Kusini ilichambua yaliyomo kwenye mifuko kutoka kwenye baadhi ya maputo na kukuta minyoo kwenye udongo.

Wizara ya Muungano ilieleza kuwa hatari ya kuambukizwa magonjwa kutoka kwa vimelea hivi ni ndogo. Kulingana na Reuters, shehena ya puto pia ilikuwa na nguo za "kimagharibi" zilizotolewa hapo awali na Korea Kusini, ikiwa ni pamoja na Mickey Mouse, Winnie the Pooh, Hello Kitty na wahusika wengine, ambazo zilikuwa zimekatwa vipande vipande.

Maafisa wa Korea Kusini walisema takataka za Kaskazini zinaonesha hali mbaya ya kiuchumi ya nchi hiyo na kuangazia "mtazamo wake wa chuki dhidi ya Korea Kusini."

Kuhusu vimelea vinavyopatikana kwenye udongo, Wizara ya Muungano ilisema huenda hilo lilitokana na matumizi ya kinyesi cha binadamu badala ya mbolea za kemikali nchini Korea Kaskazini.

Korea Kaskazini imesema mashambulizi hayo ya puto yalikuwa ya kulipiza kisasi kampeni ya propaganda ya waasi na wanaharakati wa Korea Kusini ambao mara kwa mara hutuma puto zilizobeba chakula, dawa, pesa taslimu na vipeperushi vinavyoukosoa utawala huo.

Share: