Kenya: bodaboda kuchukua hatua ya kisheria dhidi ya serikali ya nchi hiyo

Baadhi ya waendesha pikipiki (bodaboda) kutoka jijini Malindi wameamua kuchukua hatua ya kisheria dhidi ya serikali ya Kenya Kwanza, wakidai kuwa wamesahaulika katika mipango ya serikali na kusababisha hasara kubwa kifedha pamoja na matatizo ya kisaikolojia.

Kulingana na nyaraka za mahakama zilizoonyeshwa na Citizen Digital, waendesha bodaboda hao wanadai kuwa ahadi za wanachama wa chama cha kisiasa cha Kenya Kwanza zimeleta athari kubwa kwa biashara zao, na hivyo kuwasababishia hasara kubwa ya kifedha na kuharibu sifa na mwelekeo wa biashara zao.

Waendesha bodaboda hao wanasema wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa 2022, serikali ya Kenya Kwanza iliahidi kuwawezesha na kuinua maisha ya watu wanaojihusisha na biashara ya bodaboda pamoja na Mama Mboga, lakini hawajapata msaada huo kama ilivyokuwa imeahidiwa.

Malalamiko yaliyowasilishwa na waendesha bodaboda wa Malindi, Linda Jamii, na wengine, pia yanadai kwamba kaulimbiu ya Kenya Kwanza imeondolea watu wanaojihusisha na biashara ya bodaboda na Mama Mboga mapato yao kutokana na uadui unaotokana na kutofurahishwa kwa wananchi wa Kenya dhidi ya serikali ambayo wamedai imeshindwa kupunguza gharama kubwa za maisha.

Kupitia kaulimbiu ya Kenya Kwanza, waendesha bodaboda na wafanyabiashara wa Mama Mboga wanadai kuwa mapato yao yameshuka kwa asilimia 32 ambayo ni sawa na takribani Ksh. Bilioni 426 bilioni (sawa na trilioni 6.8 za kitanzania) na kuitaka Serikali isitoe kauli yoyote kuhusu biashara zao wakidai kuwa yanaweza kuwa na athari kubwa kwa haki zao na uhuru wa kufanya biashara.

Share: