Israel yaendelea na upekuzi hospitali ya ukanda wa gaza

Israel imeendeleza leo operesheni yake ya kijeshi katika hospitali kubwa zaidi huko Gaza, ikilenga kile ilichosema ni kituo cha kamandi ya Hamas kilichofichwa katika mahandaki yaliyoko chini ya hospitali hiyo.

Hospitali ya Al-Shifa inawahifadhi maelfu ya wagonjwa, madaktari na watu waliopoteza makazi katika mapigano yanayoendelea.

Meja Jenerali Yaron Finkelman, mkuu wa operesheni za kijeshi Gaza, amesema operesheni hiyo iliendelea usiku kucha.

Israel na mshirika wake mkuu Marekani wanasema Hamas imejenga mahandaki chini ya Al-Shifa madai ambayo Hamas na wakurugenzi wakuu wa hospitali hiyo wanayakanusha.

Wakati huo huo, jeshi la Israel limesema limeishambulia nyumba ya kiongozi wa ofisi ya kisiasa wa Hamas Ismail Haniyeh katika Ukanda wa Gaza, ikisema jengo hilo lilitumika kama miundombinu ya kigaidi na aghalabu lilitumika kama sehemu ya mikutano kwa viongozi wakuu wa Hamas.

Jengo hilo lilishambuliwa na ndege za kivita. Haniyeh, aliondoka Ukanda wa Gaza mwaka wa 2019 na amekuwa akiishi Qatar na familia yake kwa miaka mingi.

Share: