Hali ya utulivu yarejeshwa nchini guinea-bissau

Jeshi nchini Guinea-Bissau limesema hali ya utulivu imerejeshwa mjini Bissau kufuatia makabiliano kati ya makundi mawili ya jeshi yaliyozuka baada ya kikosi kimoja kumtoa kizuizini waziri anayetoka upande wa upinzani.

Jeshi nchini Guinea-Bissau limesema leo Ijumaa kwamba hali ya utulivu imerejeshwa kwenye mji mkuu Bissau kufuatia makabiliano ya risasi kati ya makundi mawili ya jeshi yaliyozuka baada ya kikosi cha wa ulinzi wa taifa kumtoa kizuizini waziri mmoja anayetoka upande wa upinzani.

Mapambano yaliendelea hadi leo Ijumaa asubuhi baada ya askari wa kikosi hicho kuvamia kituo cha polisi ambako Waziri wa fedha Suleimane Seidi na mkuu wa Hazina, Antonio Monteiro, walizuiliwa tangu walipokamatwa Alhamisi usiku.

Wawili hao waliwekwa rumande kuhojiwa kwa tuhuma za kutoa bila kibali kitita cha dola milioni 10 kutoka hazina ya taifa. 

Milio ya risasi ilisikika usiku kucha katika maeneo mbalimbali ya mji wa Bissau na wakaazi waliamka leo hii na kukuta vizuizi vya barabarani vilivyowekwa na wanajeshi. Hata hivyo vizuizi hivyo viliondolewa kufikia mchana wa leo na hali imerejea kuwa ya kawaida.

Share: