Ecowas wautambua utawala wa kijeshi wa niger

Jumuiya ya Uchumi ya Afrika Magharibi (ECOWAS) imeunda kamati ya viongozi watatu kusaka makubaliano na utawala wa kijeshi wa Niger juu ya kipindi cha mpito kuelekea kwenye utawala wa kiraia.

Katika mkutano wa kilele uliofanyika siku ya Jumapili (Disemba 10) mjini Abuja, Nigeria, viongozi hao wa ECOWAS waliutambua rasmi utawala huo wa kijeshi, ingawa walitaka kipindi hicho cha mpito kiwe kifupi, ili waweze kuulegezea vikwazo vya kiuchumi walivyouwekea.

Rais wa Kamisheni ya ECOWAS, Omar Touray, aliwaambia waandishi wa habari kwamba viongozi wa mataifa ya Benin, Togo na Sierra Leone, wamekabidhiwa jukumu la kuendeleza mazungumzo na baraza la kijeshi la Niger yatakayoamuwa juu ya uondolewaji wa vikwazo.

Utawala wa kijeshi wa Niger umekuwa ukisema kwamba unahitaji angalau miaka mitatu kuirejesha nchi kwenye utawala wa kiraia.

Share: