Asilimia 80 ya maelekezo ya rc makonda yametekelezwa- dc arusha

Mashauri 37 kati ya mashauri 54 yamesikilizwa na kupatiwa ufumbuzi na ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. Felician Mtahengerwa siku nne tu mara baada ya kumalizika kwa kliniki ya Mkuu wa mkoa wa Arusha Mhe. Paul Christian Makonda ya kusikiliza na kutatua kero za wananchi wa mkoa wa Arusha.

Takwimu hizo zimetajwa na Mhe. Mkuu wa wilaya ya Arusha Felician Mtahengerwa wakati alipokuwa akieleza utekelezaji wa maelekezo ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. Paul Christian Makonda aliyoyatoa kwa Ofisi yake katika utatuzi wa changamoto mbalimbali zilizoibuliwa wakati wa Kliniki ya Mhe. Mkuu wa mkoa iliyofanyika Mei 08-10 ofisini kwake Mjini Arusha.

Mkuu wa wilaya ametaja miongoni mwa mashauri yaliyoshughulikiwa ni pamoja na suala la mtoto wa miaka mitatu aliyelawitiwa kwenye Kata ya Murieti Mjini Arusha, ambapo amesema tayari wahusika wamebainika, kukamatwa na hatua za kisheria zinaendelea kuchukuliwa.


Aidha Mkuu huyo wa Wilaya Mhe. Mtahengerwa amesema Mtoto aliyeathirika na ulawiti huo tayari amekabidhiwa kwa Mganga Mkuu wa mkoa wa Arusha kwaajili ya matibabu kama ambavyo Mhe. Mkuu wa mkoa alivyoagiza.

Katika hatua nyingine Mhe. Mkuu wa Wilaya ametangaza kuanza kwa utekelezaji wa agizo la Mhe. Mkuu wa Mkoa la kuwa na kliniki ya kuwasikiliza wananchi wa Wilaya ya Arusha ambapo amesema kwa wilaya yake zoezi hilo litafanyika kwenye viwanja vya Ofisi yake kuanzia tarehe 22-24 Mei mwaka huu akiahidi pia kutoa msaada wa kisheria na kifedha kwa walioathirika na mikopo umiza na wenye mawazo ya kibiashara.

Share: