Tamasha la familia ya viziwi duniani 2024 kufanyika hifadhi ya taifa ya serengeti

Tanzania imeendelea kuaminiwa na kupewa nafasi ya kuandaa mashindano ya tamasha la watu wenye usikivu hafifu (viziwi) la 2024 ambalo linatarajiwa kufanyika katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti ambayo ni hifadhi Bora Zaidi Barani Afrika.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro usiku wa kuamkia Novemba 26, 2023 jijini Dar es salaam wakati akihitimisha tamasha hilo ambalo limefanyika kwa mara ya pili nchini Tanzania. 

“Serikali ya Tanzania inawakaribisha kwa mara nyingine tena, Tanzania ni nchi ya amani na yenye vivutio vingi vya utalii, tamasha lijalo litafanyika katika hifadhi yetu ya Taifa ya Serengeti ambayo imeshinda kuwa hifadhi Bora zaidi Barani Afrika kwa mara ya Tano mfululizo. Nchi yetu inathamini haki za watu wote na makundi yote, ulemavu sio mwisho wa maisha, tutaendelea kushirikiana nanyi wakati wote” amesema Dkt. Ndumbaro.

Katika mashindano hayo, Nashua Patience kutoka Uganda ameibuka mshindi wa kwanza na kutwaa taji la mrembo kwa mwaka 2023 huku nafasi ya mtanashati katika mashindano hayo ikinyakuliwa na Ariko David kutoka Uganda wakati Mtanzania Caroline Mwakasaka akiibuka mshindi wa nafasi ya pili kwa upande wa shindano la Mwanamitindo Bora "modal".

Kufanyika kwa mashindano hayo kwa mara ya pili mfululizo nchini Tanzania ni fursa kwa jamii hiyo kujitangaza kwa watu wote duniani bila kujali changamoto walizonazo pamoja na kutangaza vivutio vya Tanzania kupitia jamii ya viziwi kote duniani.

Akimkaribisha Waziri Dkt. Ndumbaro, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Bw. Gerson Msigwa amesema Tanzania ipo tayari kuendelea kupokea mashindano hayo mwaka 2024 akisisitiza kuwa Tanzania ni nchi ya upendo, utulivu na amani huku akibainisha kuwa kupitia Tamasha hilo Watanzania wamenufaika na kujifunza mambo mengi yaliyooneshwa na jamii hiyo kupitia ubunifu, vipaji, umoja na Mawasiliano kupitia lugha ya alama.

Share: