Mwili wa mwanamuziki malu stonch 'nuhu' unatarajiwa kuzikwa baada ya ndugu zake kuwasili wakitokea lubumbashi, dr congo

MWILI wa mwanamuziki wa FM Academia, Malu Stonch 'Nuhu' unatarajiwa kuzikwa jijini Dar es Salaam katika makaburi ya Kondo yaliyopo Ununio mara ndugu zake watakapowasili kutokea kwao DR Congo, huku mke wa marehemu akiweka bayana kwamba mumewe huyo alikuwa anaumwa kwa zaidi ya mwezi mmoja uliopita.

Mwanamuziki huyo alikumbwa na mauti jana Jumamosi baada ya kuanguka ghafla akiwa jukwaani akiimba wimbo maarufu wa 'Hadija' na alipowahishwa hospitalini kwa matibabu zaidi aligundulika ameshafariki dunia na msiba kwa sasa upo Salasala nyumbani kwake na eneo la Kinondoni linalokutanisha wanamuziki wenzake.

Akizungumza na Mwanaspoti, mke wa marehemu, Saada Nyambibo amesema Malu alikuwa anaumwa karibu mwezi mmoja uliopita na walienda Hospitali ya Rabininsia na kugundulika na alikuwa na maambukizi kwenye damu na alianza dozi hadi kufika Pasaka alikuwa amemaliza na juzi Aprili 4 alifanya sherehe ya kumbukizi ya siku ya kuzaliwa kwake.

Saada amesema alipata taarifa kutoka kwa Patcho Mwamba kuwa mumewe amefariki dunia, lakini kabla ya taarifa hiyo, Malu alirudi nyumbani saa mbili usiku kisha kutoka muda huo kwenda kazini, ila baada ya saa tatu ndio akapata taarifa hiyo ya msiba wa nyota huyo mwenye asili ya DR Congo.

Kwa sasa msiba upo nyumbani kwa marehemu Salasala wakiendelea kusubiriwa ndugu wa marehemu wakitokea Lubumbashi, DR Congo na mwili ukiwa umehifadhiwa Hospitali ya Lugalo.





Share: