Mr right msimu wa tano yarudi na ladha mpya

Dar es Salaam. Msimu wa tano wa kipindi cha Hello Mr Right unatarajia kuanza Desemba 2 ambapo vijana zaidi ya 30 watashiriki kutafuta wenza.

Mkurugenzi wa Masoko na Maudhui kutoka Startimes, David Malisa amesema tangu kuanza kwa kipindi hicho kumekuwa na mwamko wa watu mbalimbali wakiomba kushiriki wakiwemo watu maarufu. Malisa amesema vijana wengi wamefaidika na kipindi hicho chenye burudani, elimu ambapo msimu huu utakuja na upekee tofauti na awali. "Mtakubaliana na mimi kwamba shoo hii imeweza kukuwa kwa kasi sana na kupata umaarufu kwa kuongeza idadi ya mashabiki kila msimu. Na Msimu huu wa 5 unakuja na maboresho mengi makubwa zaidi ili kuongeza ladha na burudani kwa kila mtazamaji," amesema Malisa na kuongeza; "Show hii itaruka kupitia chaneli ya ST Bongo saa 4:00 usiku, visimbuzi vyetu tumevishusha bei kupitia kampeni ya Lipa Tukubusti ni fursa kwako mtazamaji kuchangamkia ili kufurahia burudani hii,"

Mwendesha kipindi hicho Godfrey Rugarabamu maarufu MC Gara amesema msimu huu vijana zaidi ya 30 watakaoshiriki watapewa elimu ya afya, mahusiano, na mambo mbalimbali kuhusu maisha. "Tutakuwa na sapraizi nyingi ikiwemo mtangazaji mpya ni maarufu sana, jukwaa lina muonekano mpya na kuwaonesha vijana waliofanikiwa kupata wenza kupitia kipindi hicho kama bado wako kwenye mahusiano, ndoa lakini pia, kujua changamoto na mafanikio yao, kwahiyo kaa kwa kutulia" amesema Gara B

Mkuu wa vipindi ST Bongo TV, Shikunzi Haonga amesema mapumziko ya kipindi hicho yalifanya mashabiki kuleta presha ya kuhakikisha kipindi hicho kinarudi.

Share: