Mazishi ya mwanamuziki Malu Stonch yatafanyika Jumamosi jijini Dar es Salaam

Balozi wa DR Congo nchini, Pierre Masala ataongoza mazishi ya mwanamuziki Malu Stonch yatakayofanyika Jumamosi katika Makaburi ya Kondo yaliyopo Ununio, Dar es Salaam.

Mwenyekiti wa wanamuziki wa Congo waishio Tanzania, King Dodoo amesema, baada ya kutokea kifo cha Malu Stonch walienda ofisi za Ubalozi wa Congo, Upanga kufanya kikao na Balozi Masala cha kupokea taarifa ya msiba.

"Amekubali kushiriki asilimia zote kwenye mazishi ya Malu Stonch ukweli tumefarijika na ameonyesha mshikamano wa hali ya juu sana baada tu ya kupata taarifa ya msiba,"alisema King Dodoo.

Mwili wa marehemu utalala nyumbani kwa marehemu (Salasala Mwisho wa Lami-Kwa Magereza)kabla ya kupumzishwa kwenye makaburini ya Kondo Ununio, Kunduchi.

Malu Stonch alifariki Aprili 6,2024 baada ya kuanguka jukwaani kwenye Ukumbi wa Target uliopo Mbezi Beach jijini Dar es Salaam akiwa anatumbuiza katika bendi ya FM Academia iliyopo chini ya Patcho Mwamba.

Uamuzi wa mazishi ya Stonchi kufanyika Jumamosi umeafikiwa baada ya kuwasili kwa kaka yake aitwaye Pierro ambaye yuko safarini kutoka DR Congo kwa ajili ya mazishi hayo ambayo yanamsubiri yeye kama mjumbe wa familia kwani awali yalikuwa yalikuwa na sintofahamu.






Share: