Dodoma: Julai 17 Aliokuwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Freeman Mbowe, ameonekana kwa mara ya kwanza hadharani kushiriki moja kwa moja katika shughuli rasmi ya kitaifa tangu kuanza kwa mchakato mpya wa maendeleo – akitoa kauli yenye uzito katika uzinduzi wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 (Dira 2050).


Katika hotuba yake iliyopokelewa kwa shangwe na wadau mbalimbali wa maendeleo, Mbowe alisisitiza umuhimu wa kuwepo kwa ushirikishwaji wa wananchi wa kawaida, vijana, wanawake na sekta binafsi katika utekelezaji wa dira hiyo, akisema kuwa "maendeleo ya kweli hayawezi kupatikana bila haki, uwajibikaji, na utawala bora."


“Dira 2050 si karatasi ya matumaini, bali ni mwaliko kwa taifa letu kutafakari, kujifunza kutoka tulikotoka, na kuamua kwa pamoja tunapotaka kwenda. Ni lazima iwe dira ya watu – siyo ya wachache,” alisema Mbowe.

Mbowe pia alisisitiza kuwa dira hiyo mpya haina budi kuzingatia:

Mageuzi ya kisiasa na kijamii

Kuboresha mfumo wa elimu na afya

Kuwekeza katika ubunifu na teknolojia

Kudhibiti rushwa na matumizi mabaya ya rasilimali

Akizungumza mbele ya viongozi wa serikali, vyama vya siasa, taasisi za kiraia na wawakilishi wa mashirika ya kimataifa, Mbowe aliongeza kuwa chama chake kiko tayari kushirikiana katika kuhakikisha dira hiyo haiishii kuwa maandiko mazuri tu, bali inatekelezwa kwa ufanisi.